Jumatano, 27 Julai 2016

MKATABA KATI YA TTCL NA BHART AIRTEL WAISHA RASMI

TT1Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya simu Tanzania (TTCL), jinsi ya mfumo wa kutoa taarifa kwa wafanyakazi unavyofanya kazi wakati alipotembelea ofisini hiyo jijini Dar es salaam.
TT2Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni  ya Simu Tanzania (TTCL) Dkt . Kamugisha Kazaura akisoma taarifa ya utendaji kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (Hayupo pichani) wakati alipoongea na uongozi wa kampuni hiyo, jijini Dar es salaam.
TT3Mwenyekiti wa bodi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) Profesa Tolly Mbwete akifafanua jambo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (hayupo pichani) wakati Waziri alipotembelea ofisi hiyo, jijini Dar es salaam.
TT4Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akiongea na Uongozi wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) wakati alipotembelea kampuni hiyo, Jijini Dar es salaam.
TT5Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni  ya Simu Tanzania (TTCL) Dkt . Kamugisha Kazaura akifafanua jambo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa wakati alipofanya mazungumzo na wafanyakazi wa kampuni hiyo,jijini Dar es salaam.
TT6Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akiongea na wafanyakazi wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL),Jijini Dar es salaam.
PICHA ZOTE NA BENJAMINI SAWE -MAELEZO
…………………………………………………………………………………………………..
Serikali imehitimisha ubia kati ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), na Kampuni ya Bhart Airtel ya India kwa kuilipa kampuni hiyo Shilingi Bilioni 14.9 na hivyo kuirudisha TTCL mikononi mwa Serikali kwa asilimia miamoja.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amesema hatua hiyo ni mkakati wa Serikali wa kuiwezesha TTCL kujitegemea ili kuzalisha faida, Kuimarisha Miundombinu yake, na kutoa gawio Serikalini.
“Tunawataka TTCL mjipange vizuri mjitangaze ili muwe kampuni kubwa na bora ya mawasiliano hapa nchini”, amesema Prof. Mbarawa.
Waziri Prof. Mbarawa amesema katika kuiongezea nguvu TTCL Serikali itawapa kituo cha  Kutunza Taarifa cha Kijitonyama (Internet Data Center) ili ikisimamie na hivyo kujipatia mapato kupitia gharama za uendeshaji na usimamizi wa kituo hicho.
Amewataka wafanyakazi wa TTCL kufanya kazi kwa bidii, kasi, uaminifu, ubunifu na kuulinda Mkongo wa Taifa ili uwawezeshe kuwa na huduma bora na za uhakika wakati wote.
“Tumetumia fedha za mkongo wa taifa kumlipa mbia mwenzenu bhart airtel ili kuiwezesha TTCL kumilikiwa na Serikali kwa asilimia miamoja hivyo changamoto inayowakabili sasa ni kufanya mabadiliko makubwa katika upande wa kutafuta masoko ili kuweza kuongeza idadi ya wateja na kufanya kazi kwa faida”, amesisitiza Prof. Mbarawa.
Aidha Prof Mbarawa amesema katika kuijali TTCL, Serikali imeipa masafa ya 1800 na masafa ya 2100 na itawaongezea masafa ya 800 yatakayowawezesha kuwa na huduma ya 4G LTE yenye  mtandao wenye kasi na hivyo kuiongezea wateja hususani katika huduma za data.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL,  Profesa Tolly Mbwete amesema TTCL imejipanga kutoa huduma zake katika maduka makubwa, hospitali, stesheni za treni, mabasi ya mwendokasi na viwanja vya ndege katika jiji la Dar es salaam na Miji mikubwa ili kuwawezesha wananchi kunufaika na huduma za mtandao na data wakati wote.
Naye,  Mtendaji Mkuu wa TTCL Dkt. Kamugisha Kazaura, ameishukuru Serikali kwa fursa mbalimbali inazoipa kampuni hiyo na kumhakikishia Waziri Prof Mbarawa kuwa katika kipindi cha miezi mitatu ijayo matokeo ya mkakati wa mabadiliko ya kibiashara yataanza kuonekana.
Dkt. Kazaura amesema kuwa tayari watumishi wenye mtazamo wa mabadiliko ya kiteknolojia wameajiriwa na wengine watapewa mafunzo ili kuhimili soko la kibiashara na kuiwezesha TTCL kunufaika na miundombinu yake iliyopo nchi nzima.
Waziri Prof. Mbarawa alikuwa akizungumza na Menejimenti na wafanyakazi wa TTCL ikiwa ni utaratibu aliojiwekea kuzungumza na wafanyakazi na taasisi zilizopo chini ya Wizara yake.

0 maoni:

Chapisha Maoni