Jumatano, 27 Julai 2016

SERIKALI YATANGAZA MAOMBI RUZUKU AWAMU III

indexNa Asteria Muhozya, DSM
Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini ambayo inatekeleza Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) imetoa taarifa ya kukaribisha maombi ya Ruzuku Awamu ya Tatu kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini.
Akizungumza katika Kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na Televisheni ya Taifa, TBC1, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, anayeshughulikia Madini, Profesa James Mdoe alisema kuwa, kiasi cha ruzuku kilichotengwa kwa shughuli hiyo ni Dola za Marekani Milioni Tatu.
Profesa Mdoe alisema kuwa, taratibu zote za kupata washindi wa ruzuku hiyo zitafanyika kwa uwazi huku zikishirikisha Vyama vya Wachimbaji vya Mikoa (REMA), lengo likiwa ni kupata walengwa stahiki kutokana na kuwa, vyama hivyo vinawatambua wanachama wao.
“Mbali na vyama vya wachimbaji, pia Serikali itashiriki kupitia ofisi zetu za Kanda zilizoko katika Mikoa yote kabla ya kufikishwa katika ngazi ya Wizara ambapo pia kutakuwa na Kamati Maalum ya kushughulikia suala hilo,”alisisitiza Prof. Mdoe.
Akizungumzia lengo la utoaji ruzuku hiyo alisema kuwa, ni kukuza mitaji ya wachimbaji wadogo na kuongeza kuwa, tayari Serikali imekwisha toa ruzuku hiyo katika Awamu Mbili, ambapo katika Awamu ya Kwanza kwa mwaka wa fedha 2013/14, Serikali ilitenga kiasi cha Dola Laki Tano (US $ 500,000), ambapo jumla ya vikundi 11 vya wachimbaji vilinufaika na kila kikundi au mchimbaji walipata kilipata wastani wa Dola Elfu Hamsini (US $ 50,000).
Akizungumzia ruzuku Awamu ya Pili alieleza kuwa, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali ilitenga takriban shilingi Bilioni 7.2, ambapo wanufaika 111 walishinda kati ya waombaji 720.
“Waombaji wanatakiwa kuwasilisha maombi yao ndani ya siku 21 kuanzia tarehe 20 Julai, 2016. Mwombaji anatakiwa kujaza nakala Tatu (3) za fomu za maombi na kuziwasilisha katika Ofisi ya madini ambapo wahusika wanafanya shughuli zao,” alisema Prof. Mdoe.
Pia alizitaja nyaraka ambazo mwombaji anatakiwa kuambatisha na maombi yake kuwa ni pamoja na;  Nakala ya leseni ya uchimbaji au biashara ya madini au leseni ya biashara iliyothibitishwa na Kamishna wa viapo;  Nakala ya Cheti na Katiba ya kuandikishwa kwa kampuni au ushirika.
Aidha, alisema nyaraka nyingine ni pamoja na Nakala za stakabadhi za malipo ya Serikali ya ada za mwaka, mrabaha na kodi; Nakala ya Cheti cha Mlipa Kodi (TIN); Mpango wa Utunzaji Mazingira (EPP) ulioidhinishwa na Afisa Madini Kanda ikiwemo taarifa ya uzalishaji kwa kipindi kisichopungua miezi sita.
Yapo mafanikio ambayo yamepatikana kufuatia Serikali kutoa ruzuku kwa wachimbaji wadogo. Baadhi ya  mafanikio ya wanufaika wa ruzuku Awamu ya kwanza ni pamoja na Kikundi cha Itandura Miners Cooperation Society cha Nyamongo  kilichoongeza uzalishaji wa dhahabu, kampuni ya Precious Decor ya Tanga inayomilikiwa na Mwanamama  inayochimba madini ya stone  ambayo sasa ni maarufu jijini Dar Es Salaam kwa kurembesha kuta .
Aidha, mbali na utoaji ruzuku, Serikali imefanya jitihada kadhaa za kuwaendeleza wachimbaji wadogo wa madini na kuhakikisha kuwa, uchimbaji mdogo unakuwa endelevu na unakua kutoka uchimbaji mdogo kwenda uchimbaji  wa Kati hatimaye mkubwa.
Kufuatia malengo hayo, tayari Serikali imetenga maeneo 35 kwa wachimbaji wadogo yenye jumla ya hekta 242,400.81 sehemu mbalimbali Tanzania Bara.
Pia, Serikali imepanga kujenga vituo saba vya mfano katika maeneo ambayo kuna uchimbaji mwingi wa madini, ambapo vituo hivyo vinatarajiwa kujengwa kati ya mwaka 2016 hadi 2018. Aidha, vituo hivyo, vitaitwa centres of excellence ambapo migodi ya mfano itajengwa na mitambo ya uchenjuaji itasimikwa ili wachimbaji wapate huduma ya kuchenjuliwa madini yao kwa gharama nafuu.
Aidha, ili kuhakikisha madini ya vito yanayochimbwa nchini yanaongezwa thamani, Serikali imefungua Kituo cha mafunzo cha Jemolojia Tanzania (TGC) kilichopo Mkoani Arusha kwa ajili ya kufundisha uchongaji na ukataji wa madini hayo ili kuyaongezea thamani.
Pia, Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), linatoa huduma ya mafunzo ya kitaalamu ya nadharia na vitendo kwa wachimbaji wadogo wa madini na kuwapatia miongozo ili kuboresha shughuli zao.
Miradi inayoweza kupewa ruzuku katika awamu ya III ni kama ifuatavyo:
 NA AINA YA MIRADI KIWANGO CHA JUU CHA RUZUKU (USD)
1 Miradi ya kuendeleza, kuboresha na kupanua uchimbaji madini au kurekebisha mazingira yaliyotokana na shughuli hizo. 100,000
2 Miradi ya kupanua na kuboresha uchenjuaji madini au kurekebisha mazingira yaliyotokana na shughuli hizo. 100,000
3 Miradi ya kuboresha teknolojia ya uchimbaji madini, uongezaji thamani au uchenjuaji usiotumia zebaki. 100,000
4 Miradi ya uongezaji thamani hususani ukataji na uchongaji madini / mawe. 100,000
5 Miradi ya wakina mama katika maeneo ya uchimbaji mdogo yenye lengo la kutoa huduma kwa wachimbaji wadogo. 15,000

0 maoni:

Chapisha Maoni