Wasanii nchini wametakiwa kuchangamkia fursa ya kazi za sanaa ambayo inadhaminiwa na British Council Tanzania.
Wito huo umetolewa leo Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye wakati wa Uzinduzi wa Fursa ya Sanaa kwa Tanzania na Afrika Mashariki ambayo Mdhamini wake ni British Council Tanzania.
Mhe. Nnauye amesema kuwa, uzinduzi wa fursa hiyo utawasaidia wasanii nchini, Mashirika mbalimbali yakiwemo Makampuni ya ndani ya Tanzania pamoja na Afrika Mashariki pamoja na Uingereza.
Amesema kuwa, fursa hiyo ni kubwa kwa wasanii nchini na kwa Taifa kwa ujumla, hivyo ameipongeza British Council Tanzania kwa kuja na wazo hilo zuri kwa manufaa ya wasanii nchini.
‘’Napenda nichukue nafasi hii kuwapongeza British Council Tanzania kwa kuwashirikisha wasanii na Makampuni mbalimbali na kuhakikisha kuwa fursa hizi zinamfikia kila msanii ndani ya Tanzania na kuwawezesha kushirikiana pamoja kwenye Sekta ya Sanaa na Utamaduni ndani ya Afrika Mashariki na Uingereza kwa ujumla’’, alisema, Mhe. Nnauye.
Ameongeza kuwa Serikali kupitia Wizara yake imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali ndani na nje ya Tanzania katika kuwawezesha wasanii katika kukuza vipaji vyao na kupata fursa zinazowawezesha kuitangaza nchi yao.
‘’Serikali inatambua changamoto zinazowakabili wasanii wetu na imejikita katika kuhakikisha kuwa inatoa fursa zilizopo kwa wasanii wetu’’.
Mhe. Nnauye amesema kuwa, Serikali itaendelea kuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba inazidi kushirikiana na British Council Tanzania na wadau mbalimbali ili kukuza vipaji vya wasanii hao.
Kwa upande wake Mkuu wa Masuala ya Sanaa Kenya na Afrika Mashariki toka British Council, Bi. Rocca Gutteridge amesema kwamba, fursa inayodhaminiwa na British Council inalenga kuwawezesha Wasanii wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla kuwa karibu kwa kushirikiana katika vipaji vyao na hivyo wameanzisha na platifomu maalum ambayo wasanii hao watakuwa wakisaidiana katika kazi zao.