Siku moja baada ya serikali kutoa taarifa ya kuvifungia baadhi ya vituo ambavyo vinatoa tiba asili
kwa sababu kuwa vimekuwa vikijitangaza kutoa tiba ya kisasa, Baraza la
Waganga wa Tiba, Ushauri na Utafiri wa Dawa Asili Tanzania (BAWATA)
limejitokeza mbele ya waandishi wa habari na kupinga agizo hilo.
Akizungumza
na waandishi wa habari, Katibu Mkuu wa BAWATA, Shariff Daudi Bin
Wiketye alisema kuwa serikali imefanya maamuzi hayo bila hata
kuwasikiliza waganga ambao wanatoa tiba katika vituo hivyo ili kupatiwa
ufafanuzi zaidi kuhusu kazi zao.
Alisema
kuwa BAWATA inaamini kuwa kufungiwa kwa vituo hivyo kunasababishwa na
ubinafsi uliopo kwa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala lakini pia
kuongozwa na watu ambao wamesoma elimu ya kisasa hivyo hawaamini kama
tiba asili inaweza kufanya kazi.
“Tunasikitishwa
sana na utendaji kazi wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala ambalo
lipo chini ya serikali na badala ya kufanya kazi kuinua tiba asili ndiyo
limekuwa mbele kukandamiza juhudi zinazofanywa na waganga wa tiba
asili,
“Bado
tunajiuliza sababu kubwa ni nini maana wamefanya maamuzi bila hata
kuwaita waganga ili wawahoji lakini tunahisi kuwa maamuzi hayo
yanafanywa sababu baraza linaongozwa na watu wanaoamini kisasa
(hospitali) au wengine wana biashara ya tiba asili hivyo wanafungia
wengine ili wao biashara yao ifanyike vizuri,” alisema Daudi.
Aidha
alisema kuwa haoni sababu ya wao kuzuiliwa kutumia jina la udaktari na
kuvaa makoti ya rangi nyeupe na hivyo kuiomba serikali kuwaruhusu
kufanya kazi zao kama awali walivyokuwa chini ya wizara ya elimu kwani
kwa sasa wanafanya kazi zao chini ya wizara ya afya ambayo wanaamini
haiwatendei haki.
“Wakati
tupo wizara ya elimu tulikuwa tunafanya kazi vizuri lakini sasa hivi
tunabanwa, niiombe serikali kupitia rais wetu Dk. Magufuli ituruhusu
kutumia jina daktari na kuvaa makoti ya rangi nyeupe, sasa hivi wanasema
hatuna vigezo lakini awali tulitumia jina na makoti hayo tunaomba
waturuhusu tena kuendelea kutumia kama awali,” alisema Daudi.
0 maoni:
Chapisha Maoni