Alhamisi, 7 Julai 2016

Bale : Hatujuti licha ya Kuaga Euro 2016



Mshambulizi wa Wales na Real Madrid Gareth Bale amesema kuwa timu yao haijuti kubanduliwa nje ya mchuano wa Euro2016 mikononi mwa Ureno katika mkumbo wa nusu fainali.
Wales wakiongozwa na mchezaji aliyegharimu kitita kikubwa zaidi duniani walikuwa wanatazamia kupata ushindi wao wa kwanza mkubwa, lakini wakaambulia kichapo cha 2-0 mjini Lyon.
''Tulijitolea kufa na kupona uwanjani, na kila mmoja wetu alikuwa na nia ya kufanikisha ndoto yetu lakini wapi,ilikuwa ni bahati mbaya tu''
Waziri mkuu wa Uingereza anayeondoka David Cameron aliwamiminia sifa kochokocho.
''Vijana wa Wales walijitoa kimasomaso, na bila shaka wamesisimua hisia kali na ushabiki miongoni wa watu wa jamhuri ya Wales na muungano wa Uingereza kwa Jumla, tunajivunia ufanisi wao huko Ufaransa kwenye kipute cha Euro2016.''

Waziri wa kwanza wa Wales Carwyn Jones alisema ni huzuni kuwa safari yao imefikia kikomo japo akakariri kuwa ilikuwa ni jambo la kujivunia kwa Wales kutinga hatua hiyo ynusu fainali.
Hii ndio iliyokuwa mara ya kwanza kwa Wales kufuzu kwa hatu hiyo.
Awali Wales walifuzu kwa hatua ya robo fainali ya kombe la dunia mwaka wa 1958.
Baada ya kutoka sare tasa kufikia kipindi cha mapumziko Cristiano Ronaldo alifuma mkwaju w kichwa kimiani kunako dakika ya 50.
Dakika tatu tu baadaye mkwaju wake ulimgonga Nani na kuelekea kimiani kwa bao la pili.

0 maoni:

Chapisha Maoni