Jumatano, 11 Mei 2016

VIKUNDI 39 VYA WANAWAKE WILAYANI MOROGORO VYAPATIWA MIKOPO YA SHILINGI MILIONI 23.8

images22Na Benedict Liwenga, MAELEZO, Dodoma.
……………………………………………….
Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro imeviwezesha Vikundi 39 vya Wanawake pamoja na Vijana vyenye wanachama 295 kupatiwa mikopo ya jumla ya shilingi milioni 23.8 kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na Wanawake.
Taarifa hiyo imetolewa leo Bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Mhe. Selemani Jafo (Mb) wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, Mhe. Tebweta Omary lililotaka kujua mpango wa Serikali wa kuzibana na kuziamuru Hallmashauri zote ikiwemo ya Morogoro Vijijini kutenga asilimia 5 ya fedha za mapato ya ndani kwa Vijana na asilimia 5 kwa ajili ya akina mama.
Mhe. Jafo amesema kuwa, katika mwaka wa fedha wa 2015/16, Serikali imetenga shilingi milioni 175 kwa ajili ya wanawake na vijana kutokana na mapato ya ndani.
Amefafanua kuwa, mkakati wa sasa wa Serikali ni kuimarisha makusanyo ya mapato ili kujenga uwezo wa kutenga fedha zaidi ambapo katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2016/17 sharti la kupitisha makisio ya bajeti ya kila Halmashauri lilikuwa ni kuonyesha asilimia 10 zilizotengwa kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na Wanawake kutokana na mapato ya ndani.
“Halmashauri zote zimeagizwa kuhakikisha fedha hizo zinapelekwa kwenye vikundi husika ikijumuisha walemavu na kusimamia marejesho yake ili vikundi vingine viweze kunufaika.
Kwa upande mwingine, Mhe. Jafo amejibu swali la Mbunge wa Geita Mjini, Mhe. Kanyasu Costantine John ambaye alitaka kujua kwanini Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Nyankimbo imabaki kuwa shule ya Kutwa wakati mazingira yake yanafaa kuwa sekondari ya Bweni ambapo alijibu kuwa shule hiyo ilijengwa chini ya Mradi wa Geita Giold Mining na kupata usajili wa Na. S.1942 mwaka 2006 ikiwa ni shule ya kutwa kwa kidato cha Kwanza hadi cha Nne.
Aidha, amesema kuwa mwaka 2012 shule hiyo iliongezewa kidato cha Tano na Sita hali iliyoifanya shule hiyo kuwa imesajiliwa ya kutwa kwa kidato cha kwanza hadi cha nne na Bweni kwa kidato cha Tano na Sita.
“Taratibu zilizotumika ili kuisajili shule kuwa ya bweni ni Halmashauri yenyewe kuwasilisha maombi Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi ili kupata kibali”, alisema Mhe. Jafo.
Aliongeza kuwa, kabla ya kupata usajili, Kamishna wa Elimu atatuma Timu ya Wataalam katika shule husika kwa ajili ya kuhakiki uwepo wa miundombinu inayohitajika ilio shule iweze kusajiliwa kuwa ya bweni.

0 maoni:

Chapisha Maoni