Mkuu
wa Wilaya ya Kinondoni Mh. Alli Hapi amemtaka mkurugenzi wa Manispaa ya
Kinondoni kuwavua madaraka wakuu wa shule za msingi 68, pamoja na
kumuandikia barua Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam kuwavua vyeo
wakuu wa shule za sekondari 22.
Hapi
alitoa maagizo hayo leo jijini Dar es Salaam baada ya Halmashauri ya
Manispaa ya Kinondoni kufanya uhakiki na kubaini kuna wanafunzi hewa
zaidi ya 5000 katika shule za msingi na sekondari katika manispaa hiyo.
“Rais
Magufuli alitoa agizo akiwa Shinyanga kwa wakuu wa wilaya kufanya
uhakiki wa wanafunzi ili kubaini kama wana sifa na vigezo vya kupewa
ruzuku ya elimu bure,” amesema.
Amesema baada ya uhakiki kufanyika ilibainikia kuwa wakuu hao wa shule walifanya udanganyifu.
“Wamefanya
udanganyifu kwa maslahi yao binafsi kufuatia hilo mkurugenzi wa
manispaa atawavua madaraka wakuu wa shule za msingi waliofanya
udanganyifu,” amesema.
Ameongeza
“Pia mkurugenzi amuandikie barua katibu tawala wa mkoa kuwavua madaraka
wakuu wa sekondari vilevile majina ya waalimu hao yapelekwe Tume ya
Utumishi ya Walimu ili hatua nyingine za kinidhamu zifuatwe,” amesema.
Amesema
wanafunzi waliobainika kutokuwa na sifa za kupata ruzuku hizo ni 3462
katika shule za msingi 68, na 2534 katika shule za sekondari 22 ambao
hawajaandikishwa kwenye kitabu cha takwimu.
“Serikali
kila mwezi inapoteza Bilioni 18.8 kwa ajili ya kugharamia elimu bure
hivyo udanganyifu uliofanywa ni ukosefu wa maadili na uzalendo,”
amesema.
0 maoni:
Chapisha Maoni