Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli
ameviagiza vyombo vya Usalama vilivyopewa jukumu la kutengeneza madawati
kujipanga zaidi ili kutekeleza kwa wakati majukumu wanayopewa.
Mhe.
Rais aliitoa kauli hiyo leo, katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es
Salaam kwenye hafla ya uzinduzi wa mpango wa ugawaji wa madawati
yaliyotolewa na Ofisi ya Bunge kwa Majimbo 155 ikiwa ni awamu ya kwanza
ya ugawaji wa madawati hayo.
Mnamo
April 11, 2016 Mhe. Rais alipokea hundi ya shilingi Bilioni Sita kutoka
Ofisi ya Bunge na kuagiza fedha hizo zielekezwe katika utekelezaji wa
utengenezaji wa madawati ambapo Magereza na Jeshi la kujenga Taifa (JKT)
walipewa jukumu la kutengeneza madawati hayo.
Aidha
Mhe. Rais amesikitishwa na kasi ambayo JKT na Magereza wametumia katika
utengenezaji wa madawati hayo, ambapo kwa miezi mitatu wametengeneza
jumla ya madawati elfu Sitini.
“Nina
wasiwasi na kasi yenu, ikiwa kwa miezi mitatu mmetengeneza madawati
elfu sitini basi kuna uwezekano wa zoezi hili la utengenezaji wa
madawati mkamaliza mwaka 2017,” alifafanua Mhe. Rais.
Aliendelea
kwa kusema kuwa, suala la madawati ni la haraka alihitaji kusubiri kwa
muda mrefu hivyo vyombo hivyo vinatakiwa kutengeneza madawati hayo kwa
uharaka kwani nguvu kazi ya kutosha wanayo.
Kwa
upande wake, Naibu Spika Mhe. Tulia Ackson amesema kuwa Ofisi ya Bunge
inategemea kugawa madawati 120,000 kwa awamu mbili tofauti ambapo awamu
ya kwanza imekamilika na jumla ya madawati 61,385 yatagawiwa kwa majimbo
155 kati ya majimbo 264.
Fedha
iliyotolewa na Ofisi ya Bunge ni Fedha iliyotokana na matunda ya mpango
wa Serikali wa kubana matumizi ambapo Ofisi ya Bunge imeweza kubana
matumizi na kubaki na Shilingi Bilioni Sita kwa mwaka wa fedha
2015/2016.
0 maoni:
Chapisha Maoni