Watu watatu wamefariki dunia mkoani Singida, katika matukio tofauti likiwemo la mzee mmoja aliyepoteza maisha baada ya kutokwa na damu nyingi kutokana na kufanyiwa upasuaji wa tezi dume na daktari feki.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoa wa Singida, ACP Thobias Sedoyeka, alimtaja mzee huyo aliyefanyiwa upasuaji wa tezi dume, kuwa ni Israel Shaban (68) mkazi wa kijiji cha Kinyambuli kata ya Nkinto tarafa ya Kirumi wilaya ya Mkalama.
Alisema Julai, 14 mwaka huu saa mbili usiku mzee Shaban alienda nyumbani kwa Joseph Msafiri anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 35 na 40 ambaye alikuwa ameigeuza nyumba yake kuwa ni kituo cha kutolea huduma za afya.
Akifafanua, alisema inadaiwa kuwa Joseph katika miaka ya nyuma aliwahi kuwa mwajiriwa wa serikali kwa nafasi ya utabibu.
Kamanda Sedoyeka alisema kutokana na uzoefu huo, baada ya kuacha kazi serikalini, huku akijiita ni daktari, aliamua kuanza kutoa tiba ikiwemo upasuaji nyumbani kwake kinyume na sheria.
“Mtuhumiwa baada ya kumfanyia upasuaji huo wa kienyeji Mzee Shaban katika sehemu zake za siri, alitokwa damu nyingi na kupelekea kuwa katika hali mbaya. Mtuhumiwa alipobaini hali hiyo, alimtekelekeza na kufanikiwa kutoroka na kukimbilia kusiko julikana. Kwa sasa tupo kwenye msako mkali ili kumkamata na kumfikisha mahakamani,” alisema.
Aidha, alisema baada ya kufanya upekezi kwenye nyumba ya dakatari feki huyo, wamefanikiwa kukamata vifaa vingi vya utabibu na dawa nyingi za kutibu binadamu.
Katika tukio jingine, Kamanda Sedoyeka alisema Julai, 17 mwaka huu saa tano asubuhi, Hamisi Salum (24) mkazi wa kijiji cha Misuna wilaya ya Mkalama, amemwua mwanafunzi wa darasa la nne shule ya msingi Mgungira wilaya ya Iramba, Sharifa Juma (12), kwa kumkata kwa panga kichwani na shingoni.
Alisema chanzo cha mauaji hayo ni mgogoro wa muda mrefu kati ya marehemu na mtuhumiwa uliosababishwa na kitendo cha baba wa mtuhumiwa kumpendelea kwa kila kitu huku Sharifa (marehemu) akiwa ni mtoto wa kambo.
“Kwa sasa tunamshikilia Hamisi kwa mahojiano zaidi na baada ya kukamilika kwa mahojiano hayo, mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma ya mauaji,” alisema.
Wakati huo huo, Sedoyeka alisema Julai, 16 mwaka huu saa 12 jioni huko mtaa wa Karakana mjini hapa, mwili wa Patrick John (34) mkazi wa Karakana uliokotwa barabarani baada ya kutupwa.
“Chanzo cha mauaji bado kinaendelea kuchunguzwa na hakuna mtu au watu waliokamatwa kuhusiana na mauaji hayo,” alisema Sedoyeka.
Imeandikiwa na Nathaniel Limu, Singida