Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amewataka Wakurugenzi Watendaji wa Halmshauri zote nchini kuondoa kero za wananchi na si kuwaongezea kero.
Hayo ameyasema leo kwenye hafla ya Kiapo cha Uadilifu wa Utumishi wa umma iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.
“Anzisheni miradi inayotatua kero za wananchi na si kuwaongezea kero, kila eneo lina kero zake hivyo jitahidini kuziondoa,”alisema Rais Magufuli.
Amewataka Wakurugenzi hao kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya wananchi kwani wamechoshwa na kero hasa kwenye ushuru na kodi zisizo za lazima, akitolea mfano mkulima wa mchicha na mpunga kutozwa kodi wakati amelima kwa ajili ya chakula chake ya kwamba hili jambo halikubaliki.
Rais Magufuli amewaambia Wakurugenzi kuwa anawaamini kwani uteuzi wao ulifanywa kwa umakini na akaonyeshwa kushangazwa na waliokuwa wakibeza uteuzi huo hasa waliosema kuwa amemteua mwenye cheti cha usimamizi wa hoteli.
“Majina kufanana si tatizo, mimi niliyemteu ni Bwana Luhende ambaye ana diploma na masters (shada ya uzamili), Bwana Luhende hebu simama wakuone na vyeti vyako,” alisema Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli amesema kuwa hakubahatisha katika kuteua Wakurugenzi hao na kuongeza kuwa kazi hiyo ameifanya kwa umakini mkubwa.
Rais amewataka Wakurugenzi kuhakikisha wanakusanya na kusimamia kodi za wananchi ili kuwaletea maendeleo na kuwaondolea matatizo ambayo yamewachosha.
Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Samia Suluhu Hassan amewataka Wakurugenzi kuwa watumishi wa watu na si watawala.
Amewaasa Watendaji hao kujifunza sheria na kanuni zinazohusiana na kazi zao na kuwataka wawe waadilifu na wachapakazi ili kuwaletea wananchi maendeleo.
Naye Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Kassim Majali Majaliwa amewataka Wakurugenzi kuwa wawajibikaji, waadilifu na waaminifu.
“Ninyi ni injini ya maendeleo katika nchi kupitia kwenye Halmashauri zenu na kazi yenu kubwa ni kusimamia watumishi katika kuleta maendeleo katika sehemu zenu,”alisema Majaliwa.
Amewataka Wakurugenzi kukusanya kodi na kuzitumia katika miradi ya maendeleo kwa uaminifu na kuwasisistiza kuzingatia thamani ya fedha katika mradi husika (Value for Money)
Jumla ya Wakurugenzi 185 wamekula kiapo cha uadilifu katika utumishi wa umma na kuhudhuria mafunzo ya maadili yaliyoandaliwa na Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.