Alhamisi, 23 Juni 2016

TOVUTI YA WANANCHI INAVYOTATUA KERO ZA WANANCHI


indexNa. Immaculate Makilika -MAELEZO
Ni ukweli usiopingika kwamba dunia imeingia katika maendeleo ya teknolojia yanayopelekea matumizi ya vifaa vya kisasa na vyenye utaalamu wa hali ya juu katika kufanya shughuli mbalimbali, ambazo hapo awali zilifanywa kwa kutumia nguvu kubwa na idadi kubwa ya watu na kwa muda mrefu.
Maendeleo hayo ya teknolojia yamejidhihirisha katika nyanja nyingi mojawapo ni hii ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano. Ukuaji wa teknolojia ya habari na mawasiliano umerahisisha mawasiliano na unatoa fursa kwa jamii kwa ujumla kuwa huru zaidi katika kutekeleza majukumu yake.
Serikali inatoa fursa kwa wananchi kutoa hoja na kero zao popote pale walipo kwa kuanzisha tovuti katika wizara, taasisi na ofisi zake ambazo zinawezesha wananchi kupata tarifa muhimu na kwa urahisi kuhusu wizara, ofisi ama taasisi husika na serikali kwa ujumla.
Katika kuzingatia maendeleo hayo ya teknolojia ya habari na mawasiliano, mwaka 2006 Rais wa awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, aliitaka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wakati huo chini ya Idara ya Habari  -MAELEZO kuanzisha, kuratibu na kusimamia Tovuti ya Wananchi.
Dhamira kubwa ya kuanzishwa kwa tovuti hii ni kutokana na matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Ibara ya 18 toleo la mwaka 2005, maagizo ya Sera ya Habari na Utangazaji ya mwaka 2003; na dhana ya Serikali inayozingatia Haki za Binadamu na Utawala Bora kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 19 ya Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu na Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano.
Aidha, tovuti hii inatoa fursa kwa wananchi kuwasiliana moja kwa moja na Serikali yao, kuwawezesha watanzania popote walipo duniani kuweza kuwasilisha hoja zao, maoni na malalamiko serikalini kwa kutumia mtandao wa intaneti .

0 maoni:

Chapisha Maoni