Ijumaa, 4 Novemba 2016

VIJANA PEMBA WATAKIWA KUTOSHAWISHIKA KUINGIA KWENYE MIGOGORO YA KISIASA

Posted by Esta Malibiche on Nov 4,2016 in NEWS

maxresdefault
 Na Masanja Mabula – PEMBA.
AFISA Mdhamini Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala bora Pemba, Massoud Ali Mohamed, amewataka Vijana Kisiwani Pemba, kutokukubali kushawishiwa kuingia katika migogoro inayosababishwa na wanasiasa na kupelekea uvunjifu wa amani ya nchi.
Alisema vijana wanapaswa, kulinda amani ya nchi yao na kuwa tayari kushiriki katika mambo yatakayosaidia nchi kupiga hatua, sio kukubali kuingizwa katika mambo yanayopelekea uvunjifu wa amani ya nchi.Wito huo aliutoa huko katika skuli ya Madungu maandalizi mjini Chake Chake, wakati alipokuwa akifungua mafunzo ya kwa Vijana 100 kutoka ndani ya Wilaya ya Chake Chake Kisiwani Pemba.
Alisema vijana kujiingiza katika migogoro hiyo ni kutokujitendea haki, hivyo wanapaswa kutokukubali kugeuzwa chombo katika migogoro ya aina yoyote ikiwemo Kisiasa, Kijamii na kiuchumi, badala yake watumike katika kujenga maendeleo ya nchi.
“Kitu kizuri duaniani ni kujitambua ndio chachu ya mafanikio sehemu yoyote duniani, Vijana wengi wanashindwa kujitambua ndio sababu inayopelekea hayo masuala ya mimba za Utotoni, Utumiaji wa madawa ya kulevya”alisema.
Mdhamini huyo alifahamisha amani iliyopo ikiharibika haitochagua aliyesababisha, aliseyemo bali kila mtu atahusika na wala hakutokuwa na kitu chochote kitakachoendelea katika nchi.
Aidha alisema vijana wamekuwa ni wahanga na waathirika wakubwa katika utumiaji wa madawa ya kulevya, Ukimwi na Mimba za Utotoni hivyo ni vyema vijana kuwa mstari wa mbele, kukataa uningizwaji wa madawa hayo ya kulevya ili kunusuru maisha yao.
Akizungumiza suala la mimba za Utotoni alisema vijana ndio waathirika kwa kufanya au kufanyiwa, hivyo wakati umefika kukemea suala hilo ili kuweza kupunguza wimbi kubwa ambalo la vijana kuingia katika majanga hayo.
“hakuna Taifa lolote linaloweza kusimama bila ya kuwa na vijana, hakuna taifa linaloweza kutumia nguvu kazi ya maana kama sio Vijana, yakiachiwa hayo dawa ya kulevya kuendelea, Ukimwi ukiendelea na mimba za Utotoni zikiendelea hakuna taifa litakalopiga hatua”alisema.
Hata hivyo aliwataka vijana kuwa mstari wa mbele kupambana na wanaoingiza madawa ya kulevya, wasambazaji, wauzaji ili kulinda vijana na ndugu zao ambao ndio tegemeo la taifa la kesho.
Mwenyekiti wa jumuiya ya JUKAMKUM Pemba, Hassan Abdalla Rashid alisema lengo la JUKAMKUM ni kuelimisha athari za madawa ya kulevya, Ukimwi na mimba za umri mdogo kwa vijana.
Alisema waathirika wakubwa ni vijana katika mada ya Kulevya, mimba za Utotoni, hivyo vijana wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kukemea suala hilo.Mratibu wa Idara ya Vijana Pemba Ali Mussa Bakari, alisema lengo ni kuwafanya vijana kuwa wajuzi wa kujitambua wao wenyewe kushiriki katika harakati za maenedeleo.
Alisema vijana wamekuwa wakifanywa ngazi ya kuingizwa katika migogoro ya siasa, jambo ambalo linathiri vijana waliowengi.“Vijana wanahitaji kupata muongozo sahihi na maelekezo ya kuwafanya wao waweze kushiriki katika harakati za maendeleo ya nchi”alisema.
Mafunzo hayo ya siku tatu kwa vijana wa Wilaya ya Chake Chake, yameendeshwa na Jumuiya ya JUKAMKUM kwa ufadhili wa The Foundation for Civili Society.

0 maoni:

Chapisha Maoni