Ijumaa, 10 Juni 2016

INTERNEWS yawafunda waandishi sheria ya ardhi

ai1MWANASHERIA kutoka taasisi ya HAKIARDHI jijini Dar es Salaam Mafole Baraka, akitoa somo kuhusu sheria ya ardhi ya Tanzania kwa waandishi wa habari katika mafunzo yaliyoandaliwa na Shirika la Kimataifa, INTERNEWS na kufanyika Wanyama Hotel, Sinza Dar es Salaam kuanzia Juni 8 hadi 9, 2016. (Picha na INTERNEWS).  
ai2MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la INTERNEWS Tanzania Wence Mushi, akifafanua jambo kwa waandishi wa habari waliopata mafunzo juu ya rasimali za gesi, mafuta na haki ya ardhi katika Wanyama Hotel jijini Dare es Salaam kuanzia Juni 8 hadi 9, 2016. (Picha na Salum Vuai-Maelezo, Zanzibar).
ai3MSIMAMIZI Mkuu wa INTERNEWS Bi. Alakok Mayombo (wa pili kushoto mstari wa mbele) na Mkurugenzi wake Wence Mushi (kushoto kwake), wakiwa katika picha ya pamoja na waandishi walioshiriki mafyunzo yahusuyo gesi, mafuta ba haki ya ardhi jijini Dar es Salaam. (Picha na INTERNEWS).
…………………………………………………………………………………………………………
Na Salum Vuai, DAR ES SALAAM
MIGOGORO mingi ya ardhi inayotokea sehemu mbalimbali nchini Tanzania, husababishwa na kutoeleweka kwa sheria ya ardhi miongoni mwa wananchi wengi.
Mwanasheria kutoka taasisi ya HAKIARDHI ya Dar es Salaam Mafole Baraka, amesema katika mafunzo ya waandishi wa habari yaliyofanyika Wanyama Hotel jijini humo, kwamba watu wengi hujikuta wakipoteza haki zao kirahisi, kwa kuwa hawaelewi chochote kuhusu sheria hiyo.
Katika mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoandaliwa na shirika la kimataifa la kuwainua waandishi wa habari (INTERNEWS), Baraka alisema migogoro hiyo imekuwa ikisababisha ugomvi kati ya wanafamilia, wanavijiji na halmashauri za maeneo husika.
Aliyataja baadhi ya mambo yanayoibua migogoro kuwa ni pamoja na kujitokeza kwa kadhia nyingi za ardhi kuuzwa zaidi ya mara moja, na wakati mwengine viongozi wa familia kuamua kuuza bila kushirikisha wenzao.  
Alifahamisha kuwa kuundwa kwa taasisi ya HAKIARDHI kumelenga kusaidia kupunguza migogoro ya aina hiyo kama si kuyamaliza kabisa.
Alibainisha baadhi ya mafanikio yaliyopatikana na taasisi yake katika kupunguza migogoro hiyo kuwa na kuweza kushawishi uundaji wa mabaraza ya ardhi ya vijiji, kusuluhisha baadhi ya migogoro, huku kesi nyengine zikiwa zinaendelea katika mahakama mbalimbali.
Aidha alisema hadi sasa wamefanikiwa kuvifikia zaidi ya vijiji elfu mbili, na kwamba wananchi wameelimika vya kutosha na kuweza kudai na kutetea haki zao mara baada kupata elimu juu ya sheria za ardhi.
“Si hayo tu, bali pia tumefanikiwa kushawishi watunga sera kuziimarisha sheria za ardhi ikiwemo kutajwa kwenye rasimu ya katiba mpya,” alieleza mwanasheria huyo.
Hata hivyo, alisema kumekuwa na changamoto kadhaa ikiwemo ya kifedha, ambayo inahitajika ili malengo ya taasisi kuifikia nchi nzima yaweze kufanikiwa.
Baraka alisema mbali na hayo, utashi wa kisiasa nao umekuwa ukichangia sana kuendelea kwa migogoro mingi ya ardhi.
Ili kuipatia ufumbuzi migogoro hiyo, alishauri kuendelea kutolewa elimu kwa wananchi, kuheshimu sheria za ardhi, kupima maeneo na kuviimarisha vyombo vya utatuzi wa migogoro hiyo.
Mapema, Mkurugenzi wa INTERNEWS Tanzania Wence Mushi, alisema ni jukumu la waandishi wa habari kutumia taaluma yao kuibua na kuelekeza njia ya kumaliza changamoto mbalimbali zinazowagusa wananchi ikiwemo migogoro ya ardhi.
Alisema tasnia ya habari ina nafasi kubwa ya kuleta mabadiliko chanya katika nchi yoyote, hivyo ni vyema wajikite katika kufanya uchunguzi na kuandika kadhia za aina hiyo, pamoja na mafanikio yanayopatikana baada ya mamlaka za juu kuzinduka kutokana na taarifa zinazoandikwa.
Katika siku ya kwanza ya mafunzo hayo, mkufunzi kutoka taasisi ya FAWOPA (Faidika Wote Pamoja) Balthazar Komba, alizungumzia kwa kina kuhusu miradi ya gesi nchini, changamoto zake na matumaini ya Watanzania kushuhudia matunda ya nishati hiyo.
Akitoa shukurani kwa niaba ya washiriki wenzake, mwandishi wa kituo cha televisheni cha Chanel Ten David Ramadhan, alisema mafunzo waliyopata yamewapa uelewa kubwa juu ya namna ya kuripoti masuala mbalimbali yanayogusa maslahi ya umma na taifa.
Alisema hiyo ni hatua muhimu na kuahidi kuwa wataongeza jitihada  katika kuibua na kuandika mambo tofauti yanayohitaji kupatiwa majibu kwa lengo ya kuinua maisha ya Watanzania.

0 maoni:

Chapisha Maoni