Ijumaa, 2 Desemba 2016

RIDHIWANI – WENYE MAAMBUKIZI YA UKIMWI WASIJINYANYAPAE

Posted by Esta Malibiche on Dec2,2016 in NEWS
img_7115
Na Mwamvua Mwinyi,Pwani
WATU wanaoishi na maambukizi ya virusi vya ukimwi wameaswa kuacha kujinyanyapaa ama kukata tamaa na badala yake wahakikishe wanajilinda na kuepuka maambukizi mapya ya ukimwi.
Aidha wametakiwa kutumia madawa ya kufubaza makali ya virusi vya ukimwi ARVs kiuhakika.
Rai hiyo imetolewa na mbunge wa jimbo la Chalinze, Ridhiwani Kikwete, huko Mdaula, wakati wa maadhimisho ya siku ya ukimwi dunia katika kituo cha kupima na kutoa elimu juu ya masuala ya ugonjwa wa ukimwi.
Alisema kuwa watu wengi wanaopima na kujikuta na maambukizi hukata tamaa na wengine kuamua hata kujidhuru.
Ridhiwani aliwapa moyo wasijinyanyapae bali wafuate maelekezo ya wataalumu ili kukinga maambukizi mapya.
Hata hivyo alisema pia ni wajibu wa jamii kuwaheshimu,kuwapa ushirikiano na kuwasaidia inapobidi ili nao wajione ni sehemu muhimu katika jamii.
Ridhiwani alitoa wito kwa wananchi jimboni humo kupiga vita maambukizi mapya ya ukimwi kwa kujilinda na kuwa waaminifu katika mahusiano yao .
“Jukumu la kujilinda ni la watu wote, tuachane na matamanio ambayo mwisho wake ni majuto “” alisema Ridhiwani.
Mbunge huyo alitumia maadhimisho hayo kuungana na wananchi wa Mdaula na baadhi ya wananchi jimbo la Chalinze kupima afya yake.
Katika maadhimisho hayo watu 81 walijitokeza kupima afya zao ambapo watu watatu kati yao waligundulika kuwa wana maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi.
Ridhiwani alianza ziara yake jimboni hapo yenye lengo la kusikiliza kero za wananchi na kutolea majibu baadhi ya hatua ambazo zinachukuliwa katika baadhi ya kero ambapo alianza na kupima afya yake kwenye maadhimisho hayo.

0 maoni:

Chapisha Maoni