Jumamosi, 3 Februari 2018

JAFO AAGIZA UDHIBITI WA MIANYA YA UPOTEVU WA MAPATO YA NDANI

Posted by Esta Malibiche ON FEBRUARI 3,2018 IN NEWS

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo akifunga mafunzo ya Uongozi kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi kinachoratibiwa OR-TAMISEMI kwa kuhsirikiana na  Taasisi ya Uongozi.

Nteghenjwa Hosseah, OR-TAMISEMI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo amewaagizi Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wote Nchini kuhakikisha wanadhibiti mianya ya upotevu wa mapato ya ndani inayotokana na  na matumizi ya mifumo ya kielektroniki.

Waziri Jafo ameyasema hayo wakati wa kufunga Mafunzo ya Uongozi kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Pwani, Lindi, Mtwara na Arusha yanayoratibiwa na OR-TAMISEMI kwa kushirikiana na Taasisi ya Uongozi na kufanyika kwa siku Tano mjini Dodoma.

Waziri Jafo amesema kuna baadhi ya Halmashauri ambazo mashine zake za Kielektroniki hazipeleki Fedha kwenye Akaunti ya Serikali na badala yake Fedha za makusanyo zimeelekezwa moja kwa moja kwenye akaunti za watu binafsi hili ni kosa kubwa sana Kisheria na linatakiwa kudhibitiwa haraka iwezekanvyo.

“Natoa mfano wa Halmashauri ya Kilindi ambayo mashine yake moja haiingizi Fedha kwenye Akaunti ya Serikali na badala yake fedha hizo zinaenda kwa watu wengine kabisa nakuagiza Mkurugenzi wa Kilindi kuwasilisha taarifa ya ununuzi wa mashine za Kielektroniki, mgawanyo wa mashine hizo kwa wahusika, matumizi yake, mchangua wa mapato yaliyopatikana kwenye halmashauri baada ya manunuzi ya mashine hizo na hatua ulizochukua baada ya kubaini kuwa mashine moja inapeleka Fedha Nje ya Mfumo Alisema Jafo.

Hili liwe somo kwa Halmashauri zote Nchini, kuhakikisha viongozi mnafuatilia mashine za kieleketroniki kama zimeunganishwa kwenye Mfumo wa Serikali na hakuna hata senti moja inayopotea katika mazingira ya kutatanisha na pia maeneo mengine yote ambayo yanaweza kusababisha upotevu wa Fedha za  Serikali.

Wakati huo huo Waziri Jafo amewatakata viongozi hao kwenda kusimamia miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao kuanzia ukarabati wa  Shule Kongwe za Sekondari, Ujenzi wa miundombinu katika Vituo ya Afya, Mradi wa uboreshaji wa Miundombinu kama Mpango Miji Mkakati(TSCP) pamoja na Uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam (DMDP)

Amesema nataka kuona Viongozi wangu mnashindana katika usimamizi wa miradi wenye maeneo yenu kila mmoja akifanya vizuri na miradi yote ikatekelezwa kwa ubora unaotakiwa tutakuwa tumewasaidia sana watanzania katika kuwafikia huduma bora na hili ndio deni letu kubwa kwa wananchi lazima tuache Alama ya Maendeleo.

“Ktika ujenzi wa miundombinu ya Afya miwsho ni Tarehe 30 nataka mradi huu ukikamilika tulete mapinduzi katika Sekta ya Afya Nchini na kwenye hili tutashidanisha Halmashauri na itakayofanya vizuri Ofisi yangu itatoa zawadi pamoja na Cheti cha Utambuzi wa usimamizi bora wa Mradi wa Ujenzi wa Vituo vya Afya.” Alisema Waziri Jafo.

Kwenye Miundombinu  msimamie ipasavyo miradi yote ya miundombinu nataka miradi hii ibadilishe Sura ya Nchi Yatu mpaka ikifika 2020 mtu aliyeondoka Nchindi miaka mitano nyuma akirudi apotee Akute Miji yetu imebadilika kwa kuwa na barabara nzuri, Taa za barabrani kila, mifereji ya kusafirishia maji ya mvua, madampo ya kisasa pamoja na Stendi za kuvutia aliongeza Jafo.

Akizungumzia mafunzo waliyoyapata Viongozi hawa Jafo amesema nategemea kutakua na mabadiliko makubwa baada ya mafunzo haya, mmejifunza mengi sasa muende mkatekeleze kwa Vitendo, mkasimamie Nidhamu ya Kazi, mkajali mipaka yeu ya kazi na mkaboreshe mahusiano kwa maslahi mapana ya kuwaletea wananchi maendeleo.

Awali akitoa Taarifa ya mafunzo haya Kaimu Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi Bw. Kadari Singo amesema mpaka sasa Taasisi ya Uongozi imekamilisha mtiririko wa kutoa mafunzo kwa Wakuu wa Wilaya na Halmashauri zote Nchini na wanaishukuru OR-TAMISEMI kwa ushirikiano walioutoa katika kufanikisha mafunzo yaliyotolewa kwa awamu nne kwa viongozi wa kanda mbalimbali.

Amesema kiongozi akipita katika mafunzo haya hawezi kuwa kama alivyokuja  mwanzoni kutakua na mabadiliko ya Kitabia ambayo yatachangia sana kuwabadilisha wananchi wataoenda kuongozwa  na zaidi Viongozi hawa watakua na uwezo mkubwa wa Kuwaza Kimkakati ambapo mipango yao itakuwa na Tija katika maisha ya wananchi wanaowaongoza.

Akitoa Neno la Shukrani Mkuu wa Wilaya ya Same Mhe.RoseMery Staki amesema mafunzo haya ni tofauti na yale waliokuwa wanapewa viongozi huko nyuma haya ni bora zaidi kwa kuwa yanagusa mtu binafsi, kisha wanagusa katika Ngazi ya Uongozi kisha kuwafundisha kama watanzania hivyo elimu waliyoipata hapa itasaidia sana katika kutatua changamoto za kila namna ambazo wamekuwa wakikabiliana nazo katika shughuli zao za kila siku.




Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo akifunga mafunzo ya Uongozi kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi kinachoratibiwa OR-TAMISEMI kwa kuhsirikiana na  Taasisi ya Uongozi.


 Kaimu Mkurugenzi wa Tawala za Mikoa kutoka OR-TAMISEMI Bi. Beatrice Kimoleta akimkaribisha Mgeni Rasmi kufunga mafunzo ya Uongozi kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi.
 Kaimu Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi Bw.Kidari Singo akitoa taarifa fupi ya namna mafunzo yalivyotolewa kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi kutoka Mikoa ya Pwani, Lindi, Mtwara, Tanga,Kilimanjaro na Arusha.
Washiriki wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi wakati wa mafunzo ya ya siku tano kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi kutoka Mikoa ya Pwani, Lindi, Mtwara,Tanga,Kilimanjaro na Arusha.


........................................................


0 maoni:

Chapisha Maoni