Jumatatu, 27 Machi 2017

WAHUDUMA 80 KATIKA SEKTA YA UTALII WAPATA MAFUNZO IRINGA

Posted by Esta Malibiche on MARCH 27,2017 IN NEWS



MKUU wa Mkoa wa Iringa Amina Masenza amewataka watoa huduma katika sekta ya ukarimu na utalii kanda ya kusini kuboresha huduma zao ili kukidhi haja soko la utalii katika ukanda huu.

Mafunzo hayo yanayotolewa na wizara ya Maliasili na utalii kwa kushirikiana na Mradi wa Kuboresha Mtandao wa Maeneo Yaliyohifadhiwa Kusini mwa Tanzania (SPANEST), yanafanyika kwa muda wa siku tatu Iringa.


Aliyasema hayo jana kwenye mafunzo ya siku tatu kwa watoa huduma wa sekta ya ukarimu na utalii,na kuhudhuriwa na  watoa huduma zaidi ya 80 wanaofanya biashara inayohudumia watalii mkoani Iringa.


Masenza alisema kuwa ili kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea hifadhi za taifa za kusini watoa huduma kwa kushirikiana na sekta binafsi hawanabudi kuinua viwango vya utowaji wa huduma.

Alisema kuwa serikali ipo katika machakato wa kuboresha miundombinu za barabara na viwanja vya ndege ili kurahisha watalii kufika katika hifadhi pamoja na vivutio vilivyopo katka ukanda wa kusini.

‘’Takwimu za mwaka 2015 zinaonesha kuwa watalii wengi zaidi walitembelea mbuga za kanda za kaskazini kuliko kanda ya kusini, kwa hiyo mafunzo hayo yatakuwa chachu ya kuboresha utoaji wa huduma katika kanda ya kusini.Hivyo basi Wizara ya Maliasili na Utalii ipo katika mchakato wa kutunga kanuni zitakazowazuia wafanyakazi wa hoteli wasio na vyeti vinavyotambulika na serikali kutoa huduma katika sekta ya utalii’’Alisema Masenza

Alisema kuwa kanuni hiyo ambayo msingi wake unalenga kuendeleza na kuboresha huduma katika ya sekta hiyo, utahusisha pia kuvibana vyuo vya hoteli na utalii ili vitoe mafunzo yanayokidhi viwango kwa manufaa ya Taifa.

“Baada ya kutungwa na kuanza kutumika kwa kanuni hizo, waajiri katika sekta hiyo watalazimika kuwaajiri wafanyakazi wenye sifa ambao wamesajiliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii,” alisema Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Utalii, alisema Masenza.


 Kwa upande wake Mratibu wa SPANEST, Godwell Ole Meing’ataki alisema changamoto hizo zimesababisha huduma duni katika maeneo ya mapokezi, chakula, vinywaji na malazi, na hivyo kuleta malalamiko makubwa sana kwa wageni.


Meing’ataki alisema SPANEST inamatarajio makubwa mara mafunzo yatakapomalizika washiriki wataweza kutambua wajibu wao ili wageni waingiapo waweze kuwahudumiwa vizuri.

“Sekta ya utalii ina changamoto nyingi, lakini eneo hili la huduma ni muhimu kwasababu linaweza kusaidia kumrudisha mgeni tena na tena na kumfanya awe balozi kwa watu wengine,” alisema Meing’ataki .

Aliongeza kuwa katika sekta ya utalii haitoshi  kuwa na hoteli kubwa tu kama itakuwa haina huduma bora kwa wageni wake.
 Awali,Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Fikira Kissimba alisema licha ya ukanda wa nyanda za juu kusini kuwa na vivutio vingi vya utalii, idadi ya watalii wanaovitembelea ni ndogo na moja ya sababu yake ni uduni wa huduma katika sekta hiyo ya utalii.


Kissimba aliishukuru wizara ya maliasili na utalii na SPANEST kwa kutoa mafunzo hayo, Kissimba alisema yatakuwa chachu katika kukuza na kuendeleza utalii kusini mwa Tanzania kwa kutoa huduma bora kwa watalii.

Aliwataka wahudumu katika sekta hiyo waache tabia ya uvivu, kufanyakazi kwa mazoea na wawe wepesi kujifunza ili kuboresha huduma zao.

0 maoni:

Chapisha Maoni