Jumatano, 31 Januari 2018

MADIWANI MAFINGA WATAKA UCHUNGUZI MANUNUZI HEWA SEKONDARI YA IHUMO

Posted by Esta Malibiche on JAN 31,2018 IN NEWS







BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga limeagiza mamlaka zinazohusika kufanya uchunguzi wa matumizi hewa ya fedha  zilizotolewa kwa ajili ujenzi wa nyumba ya mwalimu katika shule ya msingi Ihumo na atakayebainika achukuliwe hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kusimamishwa kazi.
Jumla ya Sh 2,650,000 zikiwemo Sh Milioni 2 zilizotolewa na halmashauri hiyo na Sh 650,000 zilizotoka kwenye Mfuko wa Jimbo la Mafinga Mjini, ziliingizwa katika akaunti ya shule hiyo mapema mwaka jana na matumizi yake yakafanywa kati ya mwezi Mei na Julai.
Akisoma taarifa ya mkaguzi wa ndani wa halmashauri hiyo kwenye baraza hilo juzi, diwani wa kata ya Saohill, Denis Kutemile alisema katika kipindi hicho kulikuwepo na awamu mbili ya manunuzi ya sementi na vifaa vingine vya ujenzi kwa ajili ya nyumba hiyo.
Kutumile alisema kwa kupitia risiti ya kwanza ya manunuzi hewa inaonesha jumla ya Sh 840,000 zilitumika kununua mifuko 70 ya sementi lakini katika hali ya kushangaza ilikutwa mifuko 13 tu katika stoo ya shule hiyo.
“Baada ya manunuzi hayo yalifanywa manunuzi mengine hewa ya vifaa vya ujenzi ambayo kwa kupitia risiti yake yanaonesha jumla ya Sh 650,000 zilitumika,” alisema na kutoa hoja ya kuliomba baraza hilo liamuru uchunguzi ufanyike na muhusika wa matumizi hayo hewa asimamishwe kazi.
Akipigilia msumari hoja hiyo, mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Charles Makoga alisema matumizi hayo hewa yamesababisha pia ujenzi wa nyumba hiyo usimame na akaziomba mamlaka zinazohusika zifanye uchunguzi huo haraka kwani umeathiri maendeleo ya sekta hiyo katika shule hiyo.
Wakati huo huo, baraza hilo limeagiza hatua kali zichukuliwe kwa watoa huduma wa zahanati ya Bumilahinga wanaotuhumiwa kutowasilisha kunakohusika zaidi ya Sh Milioni 2 zilizochangwa na wananchi wa kijiji hicho mwaka jana waliochangia huduma za matibabu kwa hiari kwa njia ya kadi (Tiba kwa Kadi-TIKA).
Mwenyekiti wa halmashauri hiyo alisema hiyo ni mara ya pili kwa watoa huduma wa zahanati hiyo kufanya hivyo, mara ya kwanza ikiwa ni mwaka 2016 na hivyo kusababisha walengwa kukosa huduma walizotarajia kuzipata katika kituo hicho.
“Tika ni shida katika zahanati ya Bumilahinga, watu wanachanga fedha lakini zinakaa mifukoni mwa watu na kusababisha wananchi wakose huduma za afya. Tunadhani wahusika wanatumia fedha hizo kufanyia mambo yao na kuzirudisha baada ya ukaguzi kufanyika. Baraza linataka wahusika wachukuliwe hatu kali,” alisema.
Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Rajabu Gogwa aliahidi kufuatilia utekelezaji wa maagizo hayo na lingine linaloitaka halmashauri hiyo kujitangaza kupitia vyombo mbalimbali vya habari.
Katika hatua nyingine halmashauri hiyo imeahidi kushirikiana na wadau wake wote kuendeleza mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya Ukimwi (VVU) yanayoendelea kuathiri nguvu kazi yao.

Makoga alisema halmashauri yake ni moja kati ya halmashauri za mkoa wa Iringa yenye kasi kubwa ya maambukizi hayo jambo linalotishia ustawi wa watu na maendeleo ya halmashauri hiyo.

0 maoni:

Chapisha Maoni