Alhamisi, 3 Mei 2018

SERIKALI YAAAHIDI KUKARABATI SHULE YA SEKONDARI YA WASICHANA IRINGA

Posted by Esta Malibiche on MAY 3,2018 IN NEWS

IMG-20180502-WA0274 (1)
Na. Atley Kuni OR TAMISEMI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. Seleman Jafo ameahidi kuwa  shule ya Wasichana Iringa iliyopo mkoani Iringa itafanyiwa ukarabati ikiwa ni muendelezo wa serikali katika kuzikarabati shule zake kongwe hapa nchini.
Jafo alitoa kauli hiyo akiwa njiani kuelekea Dodoma, ambapo ili mlazimu kufanya ziara yakushtukiza shuleni hapo na kuzungumza pamoja na walimu, watumishi wasio walimu pamoja na wanafunzi wa shule ya Iringa wasichana kisha kuzulu na  kujionea miundombinu mbalimbali katika shule hiyo iliyo anzishwa toka mwaka 1967.
Akizungumza mara baada yakuijionea hali ya miundombinu kwenye shule hiyo, Mhe. Jafo aliiambia jumuiya hiyo kuwa Shule ya Wasichana Iringa ni miongoni mwa shule kongwe 46 zilizopo katika mpango wa ukarabati mkubwa kwenye awamu ya pili ili kuwa na mazingira bora yakusoma na kujifunzia.
“Katika mwaka wa fedha wa 2017/18 tulikarabati shule kongwe 43 na katika mwaka huu wa 2018/19, shule hii pamoja na zingine kongwe 46 hapa nchini zitakuwa katika mpango kamambe wa kukarabatiwa kama tulivyokwisha fanya kwenye shule kama 43 za awali ambapo shule 89 zote kongwe tuwe tumezimaliza” alisema Waziri Jafo.
Sambamba na ukarabati huo Mhe. Jafo ameahidi kuzifanyia kazi changamoto zote ambazo ziliainishwa mbele yake ikiwepo upungufu wa walimu wa Fizikia na Hisabati pamoja na stahiki za walimu.
“Mama yetu Nkondola, amewasilisha  changamoto za walimu wa Hesabu na Fizikia lakini pia maslahi ya walimu, naomba niwaahidi kuwa suala hilo nimelichukua lakini niwaahidi kutuma wataalam kutoka kwenye wizara yangu pamoja na wizara zingine za kisekta kuja kufanya tathmini ya kina juu ya haya mliyo niambia” alisisitiza Waziri Jafo.
Mhe. Jafo aliwataka wanafunzi hao kusoma kwa bidii huku akitoa ahadi  mbele ya jumuia hiyo kuwa, endapo katika mitihani yao ya mwisho ya kidato cha sita watapata daraja la kwanza (DV.1) zaidi ya watahiniwa  30 wa mwaka huu kwa kidato cha sita atawandalia sherehe yakujipongeza na wale watakaopata daraja la kwanza yenye pointi kati ya 3-5 wataalikwa bungeni kwa gharama za Mhe. Waziri
Mhe. Jafo akiwa katika ziara hiyo, alikagua miundombinu ya shule ikiwapo Mabweni, Vyoo, Bwalo la Chakula, Jiko na Ofisi za Walimu na kisha kufanya mazungumzo na walimu, watumishi wasio walimu pamoja na  wanafunzi.
Huo umekuwa ni utamaduni wa kiongozi huyo mwenye dhamana na OR TAMISEMI kila anapopata fursa kutembelea mikoani kutembelea shughuli za maendeleo kwa wananchi na sekta zote ili kujionea maendeleo ya watu na shughuli zao.

0 maoni:

Chapisha Maoni